ASKOFU Mkuu Mstaafu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Donald Mtetemela amesema haoni shida nchi ikipata rais kijana wakati akizungumzia sifa za rais ajaye.
Kati ya wagombea lukuki walioonesha nia ya kuwania nafasi hiyo, vijana pekee waliotangaza kuwania nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu wa mwakani ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia Januari Makamba kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM).
Na kwa upande wa vyama vya upinzani, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema), Agosti mwaka huu alifunguka na kusema ana nia ya kuwani urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 iwapo chama chake kitaridhia.
Alitoa kauli hiyo ikiwa ni miaka miwili tangu Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema) alipojitokeza hadharani akisema kwamba hatawania tena ubunge katika jimbo hilo katika Uchaguzi Mkuu ujao na badala yake atajitosa kwenye urais.
Akizungumza na wanahabari mjini Mafinga juzi, Askofu Mtetemela alisema; “kwangu mimi umri sio hoja hata kidogo, yoyote anaweza kuwa rais, awe kijana au mzee sina shida, lakini mbali na sifa nyingine zinazotajwa ni lazima awe na sifa kuu mbili kwa mtazamo wangu,” alisema.
Akizitaja sifa hizo, alisema Rais ajaye ni lazima awe mwadilifu anayepimika kwa matendo na maneno yake lakini pia ni lazima awe na moyo wa mabadiliko kwa watu wake akiunga mkono juhudi za waliomtangulia katika kuwakwamua watanzania na umasikini.
Akizungumzia tuhuma zinazorushwa dhidi yake kwamba maoni yake katika bunge la katiba yanamuondolea sifa ya kuwa mwakilishi anayetoka katika taasisi za dini, Askofu Mtetemela alisema yeye sio mwanachama wa chama chochote cha siasa nchini na kwamba wanaomuhusisha na Chama cha Mapinduzi (CCM) kwasababu ya msimamo wake katika mchakato wa Katiba Mpya wanakosea.
“Niko katika bunge maalumu la katiba nikiwawakilisha waumini wangu, wenye itikadi tofauti. Nikiwa chama fulani sitawatendea haki lakini naitwa CCM kwasababu ya msimamo wangu,” alisema alipokuwa akizungumza na wanahabari juzi, mjini Mafinga.
Pamoja na kujinasibu hivyo, tamko la Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) lililochapishwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari vya jana, limewakana wachungaji na maaskofu walio ndani ya bunge hilo (akiwemo Askofu Mtetemela) wanaodai kuteuliwa na kuwakilisha taasisi za dini.
Katika tamko lake hilo, CCT imesema ilipeleka wajumbe tisa ambao kati yao mjumbe mmoja tia ambaye ni Esther Msambazi ndiye aliyeteuliwa.
“Viongozi wengine wa dini ya kikristo (maaskofu na wachungaji) waliopo katika bunge hilo hawakutumwa na CCT na wala CCT haina taarifa ni vipi walichaguliwa kuwa wajumbe wabunge maalumu la Katiba,” lilieleza tamko hilo
Askofu Mtetemela alisema anarushiwa madongo hayo na watu waliotaka awe upande wao na asiendelee kushiriki katika bunge hilo ili kuwafurahisha.
“Siwezi kutoka kwasababu ya kuwafurahisha watu fulani. Bunge linaendelea kisheria na akidi ya vikao vyake inaruhusu. Kwanini nitoke?” alisema.
Alisema yeye ni mmoja wa wajumbe wa bunge hilo wanaounda kundi la 201 ambao kimsingi wanawakilisha makundi tofauti ya jamii na sio vyama vya siasa ambavyo tayari vinawawakilishi wake ambao ni wabunge.
Akizungumzia maoni yanayotolewa na baadhi ya taasisi za dini kuhusu kusitishwa kwa mchakato huo  mpaka yatakapopatikana maridhiano ya pande zinazosigana;
Askofu Mtetemela alisema taarifa potofu wanazopata kutoka katika vyanzo visivyo sahihi zimepelekea yatolewe matamko yanayotaka kuhatarisha mchakato huo.
“Kuna mambo yanatokea nje ya bunge na yanaoonekana yana nguvu kwa wananchi lakini ukweli wa mambo huko ndani ya bunge. Tunaijadili rasimu na si vinginevyo, pale tunapoona pako sawa hatuna shida lakini yapo maeneo ambayo yanahitaji kuboreshwa na hiyo ndio kazi tunayofanya kwasababu maana ya bunge maalumu la katiba sio kukubali kila kitu kilicholetwa kwenye rasimu” alisema.
Alisema kinachofanywa na bunge hilo sio hitimisho la watanzania kupata katiba mpya na ni makosa kuwahukumu hivisasa kwani baada ya kazi yao, katiba hiyo itapelekwa mbele yao ili ipigiwe kura.

Post a Comment

 
Top