Kaimu Mkurugenzi wa Mkwawa Hunting Safaris, Mohamed Huwel (wa pili kulia) akieleza jinsi kampuni yake ilivyosikitishwa na tukio la wageni wake kuvamiwa na wafanyakazi wa Kilombero North Safaris.
 Zoezi la kuonesha mipaka ya wawekezaji hao lifanywa.
Diwani wa kata ya Idodi, Onesmo Mtatifikolo akieleza jambo katika tukio hilo.

WANANCHI wa kata ya Idodi wilayani Iringa wameituhumu kampuni ya Kilombero North Safaris kuingia katika mipaka ya uwekezaji isiyomuhusu na kuwabugudhi wawekezaji wengine.

Idodi ni moja kati ya vijiji 21 vinavyounda Jumuiya ya Hifadhi ya Malihai Tarafa ya Idodi na Pawaga (Mbomipa) inayopokana na Hifadhi ya Taifa ya Ruaha. 
Mwenyekiti wa  Mbomipa Phillip Mkumbata amenukuliwa mara kadhaa akithibitisha kwamba kampuni ya Kilombero North Safaris, miaka micheche iliyopita iliingia mkataba na jumuiya hiyo wa kuwekeza katika eneo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 2 katika kanda ya uwekezaji ya Lunda kwa ajili ya kujenga kambi na hoteli za kitalii.
Katika mazingira yaliyopata kuelezwa na Diwani wa Kata ya Ilolompya, Fundi Mihayo kwamba ni ya kutatanisha, mwaka 2012 wataalamu wa halmashauri ya wilaya ya Iringa na wizara ya Maliasili na Utalii waliilazimisha jumuiya hiyo kuingia mkataba wa miaka 25 na kampuni hiyo, mkataba unaopingwa na wananchi wanaounda jumuiya hiyo.
Katika tukio la hivikaribuni na ambalo limewakasilisha wananchi wa kijiji cha Idodi mwekezaji huyo aliingia katika eneo la Ilusi lililotolewa kwa kampuni nyingine ya Mkwawa Hunting Safaris Ltd kwa shughuli za uwindaji na ujenzi wa hoteli.
Septemba 5, mwaka huu, wafanyakazi watano wa Kilombero North Safaris waliingia katika eneo la Ilusi lililotolewa na kijiji cha Idodi kwa kampuni ya Mkwawa hunting Safaris na kuwakamata wageni watatu toka nchini Italia waliokuwa wakitalii na kuwinda katika eneo hilo.
Mmoja wa wafanyakazi wa Kilombero North Safaris, Charles Gwero alisema waliwakamata wageni hao na kuwanyang’anya leseni za uwindaji wakiamini kwamba eneo la Ilusi lipo ndani ya mipaka ya kampuni yao.
“Tuliwakamata wageni hao kwakuwa tulikuwa hatujui vizuri mwisho wa mipaka yetu; walipokuja wana vijiji na kutuelewesha tukawarudishia leseni zao na kufikia muafaka wa mgogoro huo,” alisema.
Kaimu Mkurugenzi wa Mkwawa Hunting Safaris Ltd, Mohamed Huwel alisema; “kitendo kilichofanywa na kampuni ya Kilombero ni cha kusikitisha kwani kinaonekana kilifanywa kwa lengo la kuchafua jina la kampuni yetu.”
Huwel alisema kampuni yao itakutana na mwanasheria wao ili waangalie uwekezano wa kuishitaki kampuni ya Kilombero kwa kuwadhalilisha wageni wao waliokasilishwa na tukio hilo.
Diwani wa kata ya Idodi, Onesmo Mtatifikolo aliishutumu kampuni ya Kilombero akisema kitendo ilichofanya dhidi ya mwekezaji mwingine katika eneo hilo kinalenga kuigombanisha Mbomipa na mwekezaji huyo.
“Sio kweli kwamba hawajui mipaka yao, tunaamini wanaijua vizuri; lakini walifanya kusudi ili kuiharibia kampuni ya Mkwawa na mwishowe Mbomipa,” alisema.
Katibu wa Maliasili wa kijiji cha Idodi, Dani Salumo alisema wafanyakazi wa Kilombero North Safaris wamekuwa na kawaida ya kuingia katika maeneo mengine katika eneo la hifadhi ya jumuiya hiyo bila taarifa.
Mwenyekiti wa kijiji cha Idodi, Musa Kigohelo aliiomba serikali kuingilia kati mgogoro wa uwekezaji unaoendelea baina yao na kampuni hiyo ya Kilombero.
Mgogoro huo kwa mujibu wa Afisa Wanyamapori wilaya ya Iringa, Rachel Nhambu umesababisha kwa muda sasa kampuni hiyo isiilipe Mbomipa ada zake za uwekezaji na hivyo kuipotezea mapato makubwa.
 “Ni jambo la kusikitisha wanaingia katika eneo la mtu mwingine na kuwabugudhi wahusika. Hata kama tuna mgogoro nao, ni lazima wafuate taratibu ili Mbomipa na vijiji vyake visikose mapato toka kwa wawekezaji wengine” alisema Mwenyekiti wa kijiji.

Post a Comment

 
Top