Bernard Murunya.

Waliokuwa watumishi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro akiwamo aliyekuwa Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka hiyo ambaye kwa sasa ni Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, Bernard Murunya wamepandishwa kizimbani jana katika Mahakama ya Wilaya ya Karatu kujibu tuhuma mbalimbali zinazowakabili ikiwamo matumizi mabaya ya madaraka wakati wakiwa watumishi katika mamlaka hiyo.
Waliofikishwa mahakamani hapo ni washtakiwa watano, mbali ya Murunya, wengine ni Leornard Minzi aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi na Victor Appolo aliyekuwa Mkuu wa Idara ya Ikolojia.
Wengine ambao mpaka sasa ni watumishi katika mamlaka hiyo ni Bruno Kawasange, Mkurugenzi wa Hifadhi na Maendeleo ya Jamii na Justice Muumba, Meneja wa Maendeleo ya Jamii.
Akisoma hati ya mashtaka mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya, Ally Mkama, mwendesha mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Hamidu Sindano akishirikiana na Richard Jacopiyo.
Waliieleza Mahakama kuwa katika tarehe tofauti kati ya Aprili na Februari, 2011 na 2012, washtakiwa walitumia madaraka yao vibaya kwa kushawishi kumpa kazi mtaalamu mshauri, Michel Duplat raia wa Ufaransa  bila kufuata utaratibu ulioelekezwa na Sheria za Ununuzi ya Umma ya Mwaka 2004, kitendo kilichosababisha Duplat kulipwa fedha za umma kinyume na utaratibu.
Washtakiwa kwa pamoja walikana mashtaka yanayowakabili, hawakutakiwa kuzungumza chochote mahakamani hapo na waliachiwa kwa dhamana na wakiamriwa kutosafiri nje ya nchi.
Kesi hiyo iliahirishwa na itatajwa tena Januari 6, mwakani kwa kuendelea kusikilizwa.

chanzo;mwananchi.co.tz

Post a Comment

 
Top